Mkuu
 wa Kikosi cha Kupambana na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa akionesha 
Cocaine zilizokuwa zimefichwa katika mkanda wa suruali aliyokuwa amevaa 
raia wa Colombia, Andres Filipe Ballesteros Uribe (28), mara baada ya 
kukamatwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini 
Dar es Salaam. 
KIKOSI cha Kuzuia na Kupambana na Dawa za 
Kulevya nchini kinamshikilia Andres Filipe Ballesteros Uribe (28) raia 
wa Colombia kwa tuhuma za kuingiza dawa hizo nchini kinyume cha sheria.
Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini 
Dar es Salaam leo, Mkuu wa kikosi hicho, Kamanda Godfrey Nzowa alisema 
mtuhumiwa huyo aliingia nchini saa nane usiku kwa ndege ya shirika la 
Ethiopian akitokea Adisi Ababa.
Alisema mtuhumiwa huyo alikutwa na Cocaine 
iliyofungwa kwenye pakiti sita tofauti na kuiwekasehemu za siri, kiunoni
 kama mkanda na nyingine tumboni.Kamanda Nzowa alisema mtuhumiwa huyo 
mwenye pasi ya kusafiria namba AP816263 iliyotolewa Julai 3,2014 nchini 
Columbia, alitoka Columbia kupitia Adis Ababa kuja Tanzania huku 
akibainisha kwamba hiyo ni njia mpya ya usafirishaji wa dawa hizo 
haramu.
“Hawa jamaa wanajaribu kubuni mbinu mpya 
kama huyu kijana alikuwa amefunga unga wa cocaine kama zilivyokuwa 
zikifungwa pipi na akazimeza… mpaka sasa ameshatoa pipi 13 kwa njia ya 
haja kubwa na anaendelea kutoa.
“…Sio rahisi kujua idadi ya mzigo aliokuwa 
nao mpaka atakapomaliza kuzitoa zote za tumboni ndiyo tunaweza kusema 
uzito wa dawa hizo na thamani yake,” alisema kamanda Nzowa.Alisisitiza 
kwamba taarifa sasa wanazopeana kwenye mtandao wao unawezesha kukamatwa 
kwa watuhumiwa huku akibainisha kuwa lengo ni kudhibiti usafirishaji kwa
 njia yoyote.
Kamanda Nzowa alisema mafanikio yanaonekana
 kwa vile kuanzia Juni 24 mwaka huu hadi Agosti 10 hakuna mtu 
aliyekamatwa akiingiza huku akibainisha kwamba umadhubuti wa mtandao wao
 umefanikisha hilo.
“Asiyeamini kwamba tumefanikiwa atujaribu 
aone… naamini tunakokwenda dawa za kulevya hasa cocaine na heroine 
zitakuwa hazipiti wala kuingia Tanzania,” alisema na kuongeza kwamba 
wanadhibiti pia ulimaji wa bangi.Kwa mujibu wa kamanda huyo lengo la 
mtandao wao ni kudhibiti sio kukamata wala kuteketeza.
Picha zote na Francis Dande.



