MAKALLA ATAKA TATHMINI MPYA BWAWA LA MWANJORO MEATU

Naibu Waziri wa Maji, Amos Makalla akikagua bwawa la Mwanjoro huku akipokea taarifa za bwawa hilo.  Bwawa la Mwanjoro kama linavyoonekana, lilianza kujengwa tangu mwaka 2009 kwa gharama ya shilingi bilioni 1.15.  Mtaalamu wa mabwawa kutoka Wizara ya Maji Inj. Ayub Shaban akimfafanulia Naibu Waziri wa Maji namana bwawa hilo linavyotakiwa kujengwa. Naibu Waziri wa Maji, Amos Makalla akiwasimamisha wataalamu wa Wizara ya Maji nakuwapa maelekezo mbele ya wanakijiji cha Jinambo mahali ambapo bwawa la Mwanjoro lilipojengwa wakati alipokuwa anahutubia
Naibu Waziri wa Maji, Mh. Amos Makalla amewaagiza wataalamu wa maji kutoka Wizara ya Maji na Sekretarieti ya Mkoa wa Simiyu kufanya tathmini mpya ya bwawa la Mwanjoro lililopo katika kijiji cha Jinamo umbali wa kilometa 35 kutoka makao makuu ya Wilaya ya Meatu Mkoani Simiyu.
Makalla alilazimika kutembelea bwawa hilo baada ya kupokea maombi ya Mkuu wa Wilaya ya Meatu Rosemary Kiring’ini kuja kujionea hali halisi ya bwawa la Mwanjoro.
Kiring’ini alisema taarifa zinazotolewa na kupelekwa Wizarani kuwa, bwawa hilo limekamilika kwa asilimia 80 si za kweli kwani Mkandarasi ametelekeza mradi na amekimbia, ilihali wananchi wanaendelea kupata tabu ya kero ya maji.
“Mh. Naibu Waziri hata hiyo asilimia 80 wanayosema imekamilika si kweli, tutakapokwenda utajionea mwenyewe hatua ya bwawa hilo ilipofika” alieleza DC. Kiring’ini.
Baada ya kufika katika bwawa la Mwanjoro na kujionea hali halisi, Makalla hakuridhishwa na hatua iliyofikia bwawa hilo na kushangazwa kwa kiasi cha pesa ambazo tayari mkandarasi ameshalipwa.
 “Siridhiki na hatua ya mradi ulipofikia na siamini kama kazi iliyofanywa inafikia thamani ya shilingi milioni 800 ambazo mkandarasi ameshalipwa” alisema Makalla.
Kutokana na hali hiyo na baada ya kujionea hali ilivyo katika mradi huo mkubwa wa bwawa, Mh. Makalla aliwaagiza wataalamu wa maji kutoka Wizara ya Maji kufanya tathmini upya ya kazi iliyofanywa, kazi iliyobaki, gharama za kazi hiyo, pamoja na muda utakaotumika katika kulikamilisha bwawa hilo.
“Nawaagiza mufanye tathmin upya ya gharama za kukamilisha kazi hiyo, kasoro zilizopo, mapendekezo, gharama za kukamilisha na muda wa utekelezaji wa shughuli hiyo na taarifa hiyo niipate wiki ijayo”. Aliagiza Makalla.
Akihutubia wananchi wa kijiji cha Jinamo Naibu Waziri Makalla aliwaahidi wanchi hao kuwa serikali itakamilisha mradi huo katika mwaka wa fedha wa 2014/2015 endapo bajeti ya Wizara ya Maji itapita.
Katika hatua nyingine Makalla hakufurahishwa na Mkandarasi wa bwawa hilo Nyakirang’ani
Construction Limited kwa kulitelekeza bwawa hili huku akiwa ameshachukua zaidi ya shilingi milioni 800 na kuahidi kuwa atahakikisha hatopata kazi katika Wizara ya Maji nchi nzima.
Bwawa la Mwanjoro lilianza kujengwa mwaka 2009 kwa gharama ya shilingi bilioni moja na milioni mia moja na hamsini chini ya Mkandarasi Nyakirang’ani Construction Limited nakwa usimamizi wa Mtaalamu mshauri Netwas Tanzania Limited.


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...