NHIF WAANZA UTARATIBU WA UCHAKUAJI WA MTU MMOJA MMOJA

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya  (NHIF) umeazimia kuongeza wanachama wake ambao kwa sasa ni asilimia 7.4 ya Wananchi wote kwa kuvisajili vikundi mbalimbali vya wajasiriamali na ushirika katika huduma za Mfuko kwa kupitia uchangiaji wa mtu mmoja mmoja.
Hayo yamo katika hotuba ya Wizara ya Afya na Ustawi wa jamii iliyosomwa Bungeni jana.
Waziri wa wizara hiyo Dk Seif Rashid alisema katika utaratibu huo, uongozi wa vikundi ndiyo utakuwa wadhamini na pia ndiyo utakaokuwa wakala wa Mfuko katika ukusanyaji wa michango na ufuatiliaji wa upatikanaji wa huduma.
 Mkakati huoumelenga kuongeza wigo wa wanufaika wa huduma za bima ya afya nchini kufikia asilimia 30 ifikapo mwaka 2015. Kwa sasa huduma hiyo imefikia asilimia 19.2.
 Vilevile, alisema Mfuko utafanya tathmini ya nne ya Mfuko ili kuangalia uhai wa Mfuko na huduma zake kwa wanachama.
Akizungumzia  utaratibu wa kugharimia huduma za afya kwa kuchangia Mfuko wa Afya wa Jamii (CHF) kwa ajili ya sekta isiyo rasmi na wananchi waishio vijijini, Waziri huyo wa Afya alisema hadi kufikia mwezi Machi, 2013 Watanzania 4,010,844 sawa na asilimia 9.2 walikuwa wamejiunga na Mfuko huo.
Aidha Dk Rashid alisema kutokana na tathmini iliyofanywa, Mfuko wa Afya wa Jamii kwa sehemu za mjini umeanza kutumika katika mkoa wa Dar es Salaam kwa kuhusisha vikundi vya uzalishaji.
Alisema katika hotuba yake kwamba katika mwaka 2014/15 utaratibu huo unaojulikana kama Tiba kwa Kadi (TIKA) unatarajiwa kuenezwa katika mikoa ya Mwanza, Singida, Ruvuma, Pwani, Tanga, Lindi na Kilimanjaro.
"Naomba nichukue nafasi hii kuwashauri Waheshimiwa Wabunge wote kujiunga na Mfuko huo ili kuwa mfano na kutoa elimu ya Mfuko huo katika maeneo yenu ili wananchi wengi waweze kujiunga. Mimi binafsi nimejiunga na Mfuko huu na nimeona faida zake hivyo nawaomba wananchi wote nchini wajiunge na Mfuko huo" alisema Waziri Rashid.
Aidha alisema Wizara imekamilisha na kuzindua Mpango Mkakati wa Matumizi ya TEHAMA katika sekta ya afya wa mwaka 2013 - 2018, ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Afya ya mwaka 2007, inayoelekeza matumizi ya mfumo endelevu wa habari na mawasiliano katika shughuli za sekta ya afya.
 Akifafanua zaidi amesema Wizara yake pia imeboresha huduma za tiba kwa njia ya mtandao - telemedicine, na kuwa hadi sasa huduma hiyo inajumuisha hospitali ya rufaa ya kanda Mbeya, Temeke, Bagamoyo, Mwananyamala, Amana, Tumbi na Hospitali ya Rufaa ya Taifa ya Muhimbili.
Katika mwaka huu wa fedha Wizara itaunganisha Hospitali za Rufaa za Kanda (Bugando na KCMC), na Hospitali maalumu (Mirembe, Ocean Road na MOI) katika mfumo wa telemedicine ili kuboresha huduma za ushauri na tiba katika mtandao na kupunguza rufaa zisizo za lazima.
Akizungumzia vyanzo  vya kugharamia huduma za afya, Dk Rashid alisema Bima za afya imekuwa moja ya vyanzo muhimu sana katika vituo vya kutolea huduma za afya na kupunguza pengo la mahitaji ya raslimali fedha kwa kiwango kikubwa.
Alisema kutokana na Ripoti ya Mapitio ya Matumizi ya Fedha za Umma (Public Expenditure Review – PER, 2012) inaonesha kwamba vyanzo mbadala vinachangia wastani wa asilimia 5 ya mapato yote ya Halmashauri kwa sekta ya afya.
" Hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2014 Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya uliwalipa watoa huduma za matibabu kiasi cha Sh. bilioni 77.7. " alisema na kuongeza kuwa:Mfuko umeanza kutekeleza utaratibu wa kuwaunganisha watoa huduma katika mtandao wa kompyuta ili wawe wanaandaa na kuwasilisha madai kwa njia ya kielektroniki.
Alisema hatua hiyo imekusuduia kupunguza muda wa malipo na kuharakisha utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa e-Health ambao Wizara iliuzindua Oktoba mwaka jana.
Nayo Kamati ya Bunge ya afya imesema ipo haja ya Huduma za bima ya afya ziwafikie wananchi wote ikijumuisha wazee, watoto, watu wenye ulemavu, yatima, wajawazito na wasio na kipato kama haki yao ya msingi.
Aidha imeitaka Serikali ibuni njia mbadala ya kupata fedha kutekeleza mradi wa ujenzi wa hospitali ya rufaa ya Kanda ya Kusini inayotakiwa kuejengwa Mtwara.
Kuhusu ujenzi na karabati wa vituo vya kutoa huduma , kamati hiyo ya kudumu ya bunge imetaka kuandaliwa kwa mikakati maalumu ili kupunguza utegemezi kwa kushirikisha wadau wa ndani
Nayo kambi ya upinzani katika hotuba yake imetaka Mifuko inayogharamia huduma za Afya (NHIF, CHF/TIKA, CBHI, NSSF-SHIB) iwekewe utaratibu wa kufanyakazi kwa pamoja.
Aidha wametaka mapendekezo ya Mfumo wa ugharamiaji huduma za afya kwa wote yawasilishwe kwa Wadau wakiwemo waheshimiwa Wabunge na waelimishwe kuhusu dhana hiyo.
Usimamizi wa Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) uimarishwe hususani katika eneo la fedha zinazochangwa na wananchi.


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...