FAHAMU MAMBO MUHIMU KUHUSU VVU/UKIMWI

Wiki hii tunaendelea kuchambua ugonjwa wa VVU/Ukimwi kama tulivyoahidi toleo la gazeti hili lililopita na tutaeleza hatua kwa hatua mpaka mgonjwa anaonekana kuwa ana Ukimwi (AIDS).
Ili mtu ajulikane kuwa ana VVU/Ukimwi atapitia hatua nne za lazima kama nitakavyoziainisha hapa.
Hatua ya kwanza hujulikana kitaalamu kama Primary HIV Infection ambapo mgonjwa hudumu nayo kwa wiki nne baada ya maambukizi. Watu walio katika maambukizi katika hatua hii ni asilimia 20 tu ya wenye maambukizi ya VVU ambao huona dalili za ugonjwa huu.

Mara nyingi walio katika hatua hii madaktari hushindwa kutambua kama mgonjwa amepata maambukizi ya VVU kutokana na dalili na viashiria vyake kufanana sana na dalili za magonjwa mengine.
Kutokana na hilo madaktari huwa makini sana kwani aliyeambukizwa akiwa katika hatua hii huweza kuonesha dalili kama vile kuvimba tezi yaani Swollen lymph glands, anaweza kuwa na homa kali, kuumwa koo, yaani Sore throat, kutokwa na vidonda mdomoni au pembeni ya mdomo, kujihisi mchovu, kujihisi maumivu sehemu mbalimbali mwilini, kutokwa na vipele mwilini na pia kutapika, kuharisha au kuumwa tumbo.
Mgonjwa mwenye dalili hizo kitaalamu hutajwa kuwa amepata ‘Acute HIV infection/Acute HIV retroviral infection.’
Hatua ya pili ya VVU/ Ukimwi kitaalamu huitwa Clinically Asymptomatic Stage na mgonjwa huweza kudumu nayo kwa miaka 10 na wengi wao hawaonyeshi dalili yoyote isipokuwa anaweza kuwa na tezi zilizovimba, yaani Swollen lymph nodes. Lakini ukweli ni kwamba kiwango cha VVU kwenye damu hupungua sana lakini mgonjwa anaweza kumwambukiza mtu mwingine.
Hata hivyo, licha ya mgonjwa kutoonesha dalili za maradhi lakini akienda kwenye vipimo vya VVU vitaonesha kwamba ana maambukizi ya ugonjwa huo katika damu yake.

Wagonjwa wa kundi hili hutakiwa kupima kwa kipimo cha wingi wa virusi vya ukimwi, yaani Viral load test kwani VVU katika mwili wanapozaliana hujificha kwenye tezi yaani lymph nodes. Kipimo hiki pia husaidia katika kumpangia mgonjwa tiba yake.
Akitoka katika hatua hiyo huja hatua inayoitwa kitaalamu Symptomatic HIV infection, hapa kinga ya mwili huzidi kudhoofika kutokana na kuongezeka kwa VVU kwani tezi na tishu zilizoathiriwa na VVU huharibika kutokana na maambukizi kuwa mwilini muda mrefu na virusi hao hubadilikabadilika na kuwa na uwezo zaidi wa kuathiri tishu na sehemu mbalimbali za mwili na hata kuziua seli zinazokinga mwili (T helper cell) kutokana na maambukizi hivyo kushindwa kuzalisha seli nyingine mpya.


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...