OFISI YA TAIFA YA TAKWIMU YATAJA SABABU ZA MFUMUKO WA BEI

 Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Bw. Ephraimu Kwesigabo akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaa kuhusu mfumuko wa bei kwa Mwezi Oktoba 2013.

Habari Na. Aron Msigwa – Maelezo.
Hali ya kuongezeka kwa bei ya bidhaa za vyakula na bidhaa zisizo za vyakula katika maeneo mbalimbali nchini imechangia  kwa kiasi kikubwa kuwepo kwa mfumuko  wa bei.
Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Bw. Ephraimu Kwesigabo akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es salaam amesema kuwa mfumuko wa bei wa Taifa kwa Mwezi Oktoba 2013 umeongezeka hadi kufikia asilimia 6.3 kutoka 6.1 za mwezi Septemba 2013 kutokana na kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma.

Amesema kuwa hali ya kuongezeka kwa mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula majumbani na migahawani umeongezeka hadi kufikia asilimia 7.3 kwa mwezi Oktoba ikilinganishwa na asilimia 6.9 za mwezi Septemba, 2013.

Kwa upande wa bidhaa zisizo za vyakula Kwesigabo ameeleza kuwa kumekuwa na ongezeko dogo hadi asilimia 6.1 kwa mwezi Oktoba 21013 ukilinganisha na asilimia 6.0 za mwezi Septemba.

Amefafanua kuwa taarifa za matokeo ya  mfumuko wa bei kwa kipimo cha mwezi zinaonyesha kuwa mwezi Oktoba ulikua asilimia 0.6 ikilinganishwa na asilimia 0.5 za mwezi Septemba kutokana na kuongezeka kwa bei za bidhaa za vyakula na bidhaa zisizo za vyakula katika maeneo mbalimbali nchini.

Amezitaja baadhi ya bidhaa za vyakula zilizochangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa mfumuko wa bei kwa kipimo cha mwezi kuwa ni pamoja na unga wa mahindi kwa asilimia 1.5, unga wa Muhogo kwa silimia 3.5, nyama kwa asilimia 1.2, kuku kwa asilimia 3.7, samaki wabichi kwa asilimia 4.1 na kuku kwa asilimia 3.7.

Bidhaa nyingine ni pamoja na samaki wakavu kwa asilimia 9.0, dagaa kwa asilimia 2.5, maziwa ya ng’ombe kwa asilimia 1.2, matunda kwa asilimia 2.9, nazi kwa asilimia 2.6, viazi vitamu kwa asilimia 4.2 na asali kwa asilimia 5.0.

Ameongeza kuwa mchango wa bidhaa zisizo za chakula zilizochangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa mfumuko wa bei kwa kipimo cha mwezi ni pamoja na mavazi ya watoto kwa asilimia 0.4, mafuta ya taa kwa asilimia 2.1 na vifaa mbalimbali vya usafi ambavyo kwa ujumla wake ni aslimia 0.4.

Hata hivyo kufuatia hali hiyo  ya mfumuko wa bei Bw. Kwesigabo ameeleza kuwa  uwezo wa shilingi ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma za jamii umeonyesha kuwa na mwelekeo imara kwa kipindi chote cha mwaka kuanzia mwezi Januari hadi Oktoba 2013.

“Napenda niwahakikishie kuwa fahirisi za bei za Taifa zimeonyesha kuwa na mwelekeo imara kwa kipindi chote, kwa hiyo uwezo wa shilingi 100 ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma umeonyesha kuwa na mwelekeo imara” amesema.

Kuhusu ulinganifu  mfumuko wa bei wa Tanzania na baadhi ya nchi za Afrika Mashariki amesema kuwa una mwelekeo unaofanana na kueleza kuwa mfumuko wa bei nchini Kenya umefikia asilimia 7.76 kwa mwezi Oktoba 2013 huku nchini Uganda Ukifikia asilimia 8.1 kwa mwezi Oktoba kutoka asilimia 8.0 za mwezi Septemba.


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...