APIGWA HADI KUFA BAADA YA KUFUMANIWA NA MKE WA MTU MKOANI KIGOMA

Kamanda wa Polisi Mkoa Kigoma, Fraisser Kashai
MTU mmoja mkulima na mkazi wa eneo la Kumsenga wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, aliyefahamika kwa jina la Yusuph Pascal, ameuawa kwa kupigwa na vitu mbalimbali katika tukio linalodaiwa kuwa ni fumanizi la mapenzi.

Kamanda wa Polisi Mkoa Kigoma, Fraisser Kashai alisema kwamba mtuhumiwa huyo wa fumanizi, aliuawa mwanzoni mwa wiki hii.
Alisema baada ya kifo chake, mume wa mwanamke aliyefumaniwa kwa kushirikiana na watu wengine, waliuchukua mwili wa marehemu na kuutupa eneo la Mnarani mjini Kasulu.
Kufuatia tukio hilo, kamanda huyo alisema watu watano wanashikiliwa na jeshi hilo, wakituhumiwa kuhusika na tukio hilo la mauaji ya mkulima huyo.
Kashai aliwataja watu waliokamatwa kwenye tukio hilo kuwa ni watu watatu wa familia moja, ambao ni Augustino Adrian, Laurent Adrian na Peter Adrian, ambao ni wamiliki wa nyumba yalipotokea mauaji.
 
Aliwataja wengine waliokamatwa kuhusiana na tukio hilo kuwa Mihosho Hamza, ambaye ni mume wa mwanamke aliyefumaniwa akiwa ni mpangaji katika nyumba yalikotokea mauaji na Raymond Shirima.
Akisimulia kuhusu tukio, Mkuu wa upelelezi na makosa ya jinai mkoa Kigoma, David Kisusi alisema awali marehemu akiwa katika nyumba ambayo mwanamke aliyefumaniwa naye alikuwa akiishi, alivamiwa na watuhumiwa, ambao walimpiga na vitu vizito na kufariki.
Alisema baada ya kuona kuwa mtuhumiwa huyo wa fumanizi ameuawa, mume wa mwanamke huyo na watuhumiwa wengine wanne, waliuchukua mwili wa marehemu na kwenda kuutupa eneo la Mnarani ili kupoteza ushahidi.
Alisema polisi walipofika eneo ambalo mwili huo wa marehemu ulikuwa umetupwa, walianza uchunguzi wao na kubaini kuwa ulitupwa hapo baada ya kuuawa eneo lingine.
Ndipo walipofuatilia michirizi ya damu hadi katika nyumba hiyo na kukuta katika moja ya vyumba hivyo, kuna eneo limemwagiwa mchanga mwingi ili kuficha damu hiyo ya marehemu.
Habari Leo


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...