Chuo kikuu chadaiwa kuwatapeli wanachuo 115




TAASISI ya Sayansi ya Afya ya Chuo Kikuu cha Eckernforde Tanga, inatuhumiwa kuwatapeli wanachuo zaidi ya 115 iliyowadahili na kukaa chuoni hapo miezi sita kisha kuwafukuza kwa madai kuwa hawana vigezo vinavyotakiwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.

Hata hivyo, wanachuo hao walifukuzwa baada ya kuwa wamelipa ada, fedha ya chakula, malazi na michango mingine.

Kwa mujibu wa nyaraka mbalimbali ambazo Tanzania Daima limeziona, chuo hicho kilitangaza nafasi hizo kupitia gazeti la Mwananchi la Oktoba 31, 2012.

Tangazo hilo lilisomeka; “Wito wa maombi kwa ajili ya kujiunga na kozi za cheti na stashahada za sayansi za afya mwaka wa masomo 2012/2013.”

Kwa mujibu wa tangazo hilo, waombaji wangesoma kozi hiyo kwa miaka miwili ngazi ya cheti, huku wale ngazi ya stashahada wakisoma kwa miaka mitatu.

Sifa zilizoainishwa katika tangazo hilo ni kwamba mwanafunzi atakayesajiliwa ni aliyefaulu masomo manne, likiwemo moja la sayansi.

“Mwombaji lazima awe na ufaulu wa pasi tatu katika masomo ya sayansi, walau daraja ‘D’ katika kemia, biolojia na hisabati au kidato cha sita akiwa na pasi moja daraja ‘E’ katika somo lolote la sayansi,” lilisomeka tangazo hilo.

Kila fomu ya kujiunga ilinunuliwa kwa sh 20,000 ambapo fedha hizo zililipwa kupitia benki ya NBC Tawi la Tanga, akaunti na 0201030006036.

Baada ya wanachuo hao kudahiliwa kwa sifa zilizoanishwa, walisoma kwa miezi sita na wakati wakiendelea na masomo, Wizara ya Afya ilileta vigezo tofauti na vile vilivyokuwa vimeainishwa kwenye tangazo la awali.

Hatua hiyo ilisababisha wanachuo 115 kuonekana hawana sifa, na hivyo kutakiwa kuondoka au kufanya mitihani upya ili kuweza kukidhi sifa stahiki.

Badala ya kufuata masharti ya wizara, Januari 2013, uongozi wa chuo uliwatoa wasiwasi wanachuo kwa kuwaeleza kuwa hakuna suala la kujisajili kwa mara nyingine kwa kuwa chuo hicho kipo chini ya Baraza la Elimu ya Ufundi (NACTE), na kwamba wanatambuliwa.

Licha ya kupewa matumaini hayo, lakini Juni mwaka huo, walionekana hawana sifa na hivyo kuondolewa chuoni hapo kwa mizengwe.

Chanzo chetu kilidokeza kuwa waliombwa na uongozi wa chuo kutofanya fujo ili madai yao yashughulikiwe kwa utaratibu, hivyo walipewa hundi kwenda benki kuchukua fedha.

Hata hivyo, walipofika benki ya CRDB Tawi la Tanga, walielezwa kuwa hundi hizo ni feki na waliporejea chuoni, walikuta ulinzi umeimarishwa, wakalazimishwa kuondoka maneo hayo.

Baada ya kufanyiwa utapeli huo, wanachuo hao walitoa taarifa kwa Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Tanga Mjini, wakiomba kuandamana ili wafike kumwona Mkuu wa Mkoa kumweleza kilio chao.

Licha ya maandamano hayo, hakuna hatua iliyochukuliwa na Serikali ya Mkoa wa Tanga dhidi ya chuo hicho, hali iliyowalazimu kuondoka kurejea majumbani kwao wakiwa wanadai fedha hadi leo.

Wanachuo hao wanadai fedha walizolipa kwa ajili ya chakula, malazi na vifaaa vya darasani ni sh 1,987,500 kila mmoja.

Pia zipo gharama za usafiri kwa kila mmoja kutegemeana na mahali alikotoka, fedha za usumbufu na hivyo kufanya madai yote kwa pamoja kufikia sh 353,069,600.

Mbali na madai yao kufikishwa kwa mkuu wa mkoa bila kupatiwa ufumbuzi, pia wanachuo hao wamewahi kumwandikia barua Waziri Mkuu, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii na Baraza la Elimu ya Ufundi, ingawa hakuna walikosikilizwa.

Alipotafutwa Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Chuwa Kiango, alitetea kuwa suala linaloulizwa silo bali kuna tatizo jingine, huku akiomba apewe muda kwa vile alikuwa akiingia kikaoni.






“Chunguza upya, muulize aliyekupa taarifa hii, nitakupa maelezo nikitoka kwenye kikao,” alisema Prof. Kiango ingawa baadaye alipopigiwa simu hakupokea.


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...