LUIS SUAREZ AFUNGULIWA MASHITAKA YA KUMNG'ATA GIORGIO CHIELLINI UWANJANI, TAZAMA VIDEO YA TUKIO HILO

Kamati ya nidhamu ya shirikisho la soka duniani FIFA imemfungulia mashataka mshambuliaji wa timu ya taifa ya Uruguay Luis Suarez kufuatia tukio la kumng’ata beki wa timu ya taifa ya Italia Giorgio Chiellini, wakati wa mchezo wa mzunguuko wa tatu wa kundi la nne ambapo The Azzuri walikubali kufungwa bao moja kwa sifuri.

Kamati ya nidhamu imethibitisha kumfungulia mashtaka mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 26, baada ya kupata ripoti ya mchezo huo ambao ulichezwa kwenye uwanja wa das Dunas, uliopo mjini Natal.

Hata hivyo kamati hiyo imetoa nafasi kwa Luis Suarez, pamoja na shirikisho la soka nchini Uruguay kuwasilisha utetezi wao kabla ya kuanza kusikilizwa kwa kesi hiyo.

Nafasi kwa Suarez pamoja na shirikisho la soka nchini Uruguay kuwasilisha vielelezo vya ushahidi wa kupinga suala hilo, imetolewa hadi saa kumi na moja jioni kwa saa za nchini Brazil.

Tayari kocha mkuu wa timu ya taifa ya Uruguay Oscar Tabarez ameshajiondoa kwenye ushahidi huo, baada ya kukiri hakuliona tukio hilo ambalo lilijitokeza katika kipindi cha pili cha mchezo huo.

Tukio la Suarez kumng’ata Chiellini lilitokea dakika kumi kabla ya mchezo wa Italia na Uruguay haujamalizika, ambapo picha za televisheni zilionyesha kwa kurudia rudia tukio hilo ambalo linadaiwa huenda lilikuwa halali kwa mshambuliaji huyo wa klabu ya Liverpool kuonyeshwa kadi nyekundu.


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...