MAMA MJAMZITO AFUKUZWA WODINI AJIFUNGULIA KWENYE KOKOTO

 Kulia ni Rhoda Mwakyusa(50), akifuatiwa na mwanaye Sabina Mwakyusa Mwafyela(28), mume wa Sabina na Dada yake Sabina kushoto.
 Sabina Mwakyusa(28) anayedai alifukuzwa na manesi wodini na kujifungulia nje ya geti usiku huku mvua ikinyesha akiwa na Mama yake mzazi, Rhoda Mwakyusa(50).
 
 Mtoto aliyezaliwa usiku nje ya geti la Hospitali ya Ifisi Mbalizi, baada ya mama yake kudaiwa kufukuzwa akiwa na uchungu.

*Walinzi wamsaidia.
Na Gordon Kalulunga, Mbeya
HOSPITALI teule ya wilaya ya Mbeya(Ifisi-Mbalizi), imekumbwa na kashfa ya kufukuza wajawazito wodini kisha wajawazito hao kujifungulia katika mazingira yasiyo na staha nje ya hospitali.
Tukio la hivi karibuni limetokea usiku wa Desemba 19, mwaka huu, ambapo baadhi ya wauguzi waliokuwepo katika chumba cha matazamio ya kujifungua, wanadaiwa kumfukuza na kumpiga mjamzito Sabina Mwakyusa(28) mkazi wa Kijiji cha Iwala, kata ya Utengule Usongwe wilayani humo.
Akizungumza na kalulunga media blog, Sabina, alisema alifika hospitalini hapo Desemba 18, mwaka huu na alipimwa na manesi ambapo walimwambia kuwa hawamuoni mtoto tumboni mwake.
‘’Baadaye akaja Daktari na kunipima, akaniambia mtoto anaonekana vizuri na ningejifungua mtoto wa kike ndipo nikaendelea kusubiri uchungu zaidi’’ alisema Sabina.
Alisema ulipofika usiku wa Desemba 19 majira ya saa mbili usiku, alianza kujisikia uchungu, ndipo manesi waliompima mwanzo wakamwambia anatakiwa apimwe tena jambo ambalo alikataa kwa madai kuwa alikuwa akiumizwa, ndipo wakamwambia aondoke hospitalini hapo kwasababu ana kiburi.
‘’Baada ya kuonekana mimi nasita kuondoka, wakaanza kunipiga na kunipatia biki na kunilazimisha kuandika kuwa mimi sitaki kujifungulia hapo ndipo tukatoka na mama na kwenda nje ya geti na kujifungulia getini huku mvua ikinyesha’’alisema Sabina Mwakyusa.
Alisema, mama yake na baadhi ya wajawazito waliokuwepo ndani ya wodi hilo, walijaribu kuwabembeleza wasimfukuze lakini walikataa.
Mama mzazi wa mwanamke huyo, Roda Mwakyusa(50), alisema anaumia akikumbuka yaliyomkuta mwanaye ikiwa ni uzao wake wa kwanza.
‘’Niligaragara mweeeh! kuwaomba msamaha wale manesi ili wamsamehe na kumhurumia huyu mtoto wangu, lakini walikataa wakisema kuwa ana kiburi sana’’ alisema Prisca Mwakyusa.
Alisema walipotoka wodini huku mwanaye uchungu ukimzidi, walifika getini akazidiwa. Chupa ikapasuka. Damu zikaanza kumvuja; alikaa muda mrefu zaidi ya saa moja na kuanza kujifungua ndipo walinzi wa kampuni ya Mult-Lion, wakamsaidia kumpeleka katika upenu wa duka la hospitali hiyo ili kukwepa kokoto zilizopo na mvua iliyokuwa ikinyesha.
Mkurugenzi wa kampuni ya ulinzi ya Mult-Lion, Kinanda Sanga, alipoulizwa kuhusu tukio hilo, alisema kuwa hakuwa na taarifa lakini baada ya kuwauliza askari wake walimpatia taarifa ya tukio hilo kuwa lilitokea na wao wakatoa msaada.
Dada wa msichana huyo, Enitha Mwakyusa(35), alisema alipigiwa simu majira ya saa tano usiku na mama yake mzazi akimweleza yaliyomkuta mdogo wake na kwamba atafute gari la kwenda kuwachukua.
‘’Mama alinipigia simu usiku, nikawaamusha majirani ambao walikuwa na namba za madereva tax, ambapo saa saba walifika hapa nyumbani Mapelele’’ alisema Enitha.
Wifi wa Sabina Mwakyusa, Prisca Nafred, alisema alimpeleka mtoto aliyezaliwa katika hospitali hiyo majira ya saa saba mchana ya Desemba 20, kwa ajili ya chanjo, lakini hakupata chanjo kwa madai kuwa alikuwa amechelewa kufika, hivyo alitakiwa kufika siku ya Jumanne Desemba 24, mwaka huu.
Desemba 21, familia hiyo ilimpigia simu Mwandishi wa habari wakimweleza kuhusu maendeleo mabaya ya mtoto ambapo Mwandishi wa habari hizi alimtaarifu Mratibu wa afya ya mama na mtoto mkoa wa Mbeya, Prisca Butuyuyu, kuhusu suala hilo ambapo makubaliano yaliafikiwa kuwa mtoto apelekwe Hospitali ya Rufaa, kitengo cha wazazi Meta.
Mtoto huyo alipokelewa Meta na kuingizwa kwenye chumba cha joto kisha kuanza kupatiwa matibabu kwa kuwekewa drip za maji mpaka Desemba 23 mwaka huu.
Mganga Mkuu wa wilaya ya Mbeya Louis Chomboko, alipopata taarifa, alichukua hatua ya kwenda kumuona mtoto huyo katika hospitali ya Meta.
‘’Nimeonana na mama wa mtoto na kumuona mtoto chumba cha joto na kupata maelezo yote ikiwa ni pamoja na maelezo ya file la Meta hivyo nipe nafasi tena kufuatilia tukio hili hospitali ya Ifisi na tukibaini ukweli tutachukua hatua’’ alisema Dr, Chomboko akimsihi Mwandishi kutoandika kwanza habari hii.
Mganga mkuu wa hospitali ya Ifisi Mbalizi, Msafiri Kimaro, Desemba 23, mwaka huu, alipotakiwa kuzungumza na mwandishi wa habari, aliitisha kikao cha wauguzi wanne waliokuwepo siku ya tukio, Muuguzi mkuu, muuguzi kitengo cha chanjo idara ya Mama na mtoto na katibu wa hospitali hiyo.
Alisema katika hospitali hiyo, wanawake zaidi ya 300 wanajifungulia hapo lakini tukio kama hilo hakumbuki kuwahi kujitokeza ingawa Muuguzi mkuu alikiri kuwa anayeonekana kukataa kupata huduma hapo anaandika maelezo na kuruhusiwa kuondoka.
Dr. Kimaro, aliwauliza wauguzi waliokuwepo siku ya tukio, ambapo walikubali kumfahamu mjamzito huyo na kukubali kuwa alikuwa chini yao na kwamba alikataa kupata huduma hospitalini hapo na kuamua kuondoka.
‘’Ilipofika saa mbili alipatwa uchungu na tulipotaka kumpima kwa kumwingiza vidole sehemu za siri alikataa na pia siku ya kwanza alitusumbua sana na kubana miguu, ndipo akaandika maelezo mafupi kuwa hakutaka kupimwa bali kwenda yumbani kwake’’ alisema Tumaini Mgimwa.
Aliongeza kuwa mama yake mzazi wa Sabina, alimbembeleza mwanaye ili akubali lakini alikataa ndipo mama yake akaanza kulia akimtaka akubali lakini hakuweza kukubali kutibiwa hospitalini hapo.
‘’Muuguzi mkuu wa hospitali hiyo, Sikitu Mbilinyi, alisema yeye alikuwepo siku hiyo na alipoitwa akakutana na mgonjwa lakini mjamzito huyo alikataa kutibiwa ndipo akawaambia manesi kuwa mgonjwa asiondoke mpaka asaini kuwa hataki kutibiwa’’ alisema Mbilinyi.
Alisema mgonjwa kukataa au kukubali kupewa huduma na hospitali au daktari fulani ni haki yake lakini wengi hawajui haki zao na kwamba mjamzito huyo alipojifungulia katika geti la hospitali hiyo, mama yake angepaswa kuingia ndani ambako anadai eti wangempatia msaada.
Katibu wa hospitali hiyo, Goodluck Lession, alisema swali la msingi ni kwamba iweje mjamzito afike tangu Desemba 18 mpaka usiku wa kuamkia Desemba 20, kisha aseme kuwa hataki kupata huduma hospitalini hapo?
Goodluck, alisema hayo baada ya swali kutoka kwa mwandishi kumhoji muuguzi mkuu Mbilinyi swali hilo.
Kwa upande wa kiongozi wa kitengo cha chanjo hospitalini hapo, alisema kuwa kukataliwa chanjo mtoto huyo ni kutokana na dawa ya chanjo inatakiwa chupa moja kuchanjwa watoto kumi.
‘’Tunafanya hivyo kwasababu endapo mtu ukichanja mtoto mmoja, inatakiwa dawa hiyo uiandikie maelezo hivyo tunaogopa’’ alisema kiongozi huyo.
Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya kanisa la Uinjilisti Tanzania, ambalo linamiliki hospitali hiyo na serikali kuingia ubia,  Tito Nduka, alipohojiwa kuhusiana na jambo hilo, alisema kuwa amepata taarifa kuwa hospitali imeshusha ufanisi wa kazi.
‘’Kwanza kamati kuu yetu imepata taarifa za kudhorota kwa huduma kwa ujumla, lakini Mganga mkuu ni mwadilifu na msikivu, katika jambo hilo tutakaa na viongozi na kulikemea’’ Alisema Nduka.
Katibu Mkuu wa maendeleo ya kanisa hilo, JaCkob Mwakasole, alisema taarifa za kushuka kwa ufanisi wa huduma katika hospitali hiyo wamezipata na kwamba tukio hilo haliwezi kupita hivi hivi.
Mratibu wa afya ya Mama na mtoto mkoa wa Mbeya, Prisca Butuyuyu, alisema kuwa….
Mganga mkuu wa mkoa wa Mbeya, ………. Seif Mhina, alisema kuwa…
Baadhi ya wauguzi na madaktari wa hospitali hiyo ambao hawakutaka majina yao kuandikwa, wamekiri kuwepo kwa udhorotaji wa huduma za afya katika hospitali hiyo tangu ubia wa serikali na kanisa  na kwamba mpaka sasa kuna maelewano hasi kati ya waajiriwa wa serikali na wale wa kanisa jambo ambalo wanaoumia ni wagonjwa.
Wakati hayo yakiedelea kutokea nchini, malengo ya milenia yanaeleza kutaka kupunguza vifo vya mama na mtoto ifikapo mwaka 2015.
Hayo yanabainika katika utafiti wa umoja wa Mataifa, unaongelea “ndoto” ya kufikia malengo nane ya Maendeleo ya Milenia (MDGs) zaidi katika afya: kupunguza vifo vya watoto wachanga (Lengo la 4), kuboresha afya ya wajawazito (lengo la 5) na kukabiliana na VVU/UKIMWI, malaria na magonjwa mengine (Lengo 6).
Baadhi ya viongozi wa dunia wanaoongoza mtandao wa kutoa         msukumo wa kisiasa ni pamoja na Rais Michelle Bachelet wa Chile,  Rais wa Msumbiji Armando Guebuza na Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete.
Daktari bingwa nchini katika masula ya uzazi, Dr. Moke Mgoma, kutoka shirika la Evidence for action(E4A), alipohojiwa alisema alichotendewa Sabina Mwakyusa, ni kitendo kibaya ikizingatiwa kuwa serikali inafanya jitihada kuondoa ukatili wa baadhi ya wauguzi.
Mwezi Desemba mwaka 2012, Mama mmoja(jina tunalo), aliyekuwa anaumwa BP, alichomwa sindano (dawa)ambazo haziendani na ugonjwa wake na mmoja wa watoto wake alipohoji kwa uongozi wa hospitali hiyo alijibiwa kuwa hapaswi kugombana na wauguzi! Kisha akaitwa Dr. Kenneth, ambaye aliamua kuokoa maisha ya mama huyo katika hospitali hiyo ya Ifisi kwa kumchoma sindano ya dawa iliyokuwa ikitakiwa.
–KALULUNGA–


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...