Kaseja majanga... awa chaguo namba tatu jangwani

 
Kipa wa Yanga, Juma Kaseja.
Na Phillip Nkini
KIPA wa Yanga, Juma Kaseja, amesema yeye ni mzima wa afya na kukosekana kwake kwenye mechi dhidi ya Ashanti siyo ishu kubwa, lakini kocha wake amesisitiza aliamua kumfanya chaguo la tatu kutokana na kiwango.

Kaseja alijiunga na Yanga baada ya kumaliza mkataba wake na Simba na kukaa nje nusu msimu bila kucheza, lakini juzi ukiwa ndiyo mchezo wa kwanza wa mzunguko wa pili wa ligi kwa timu hiyo, hakuwepo hata kwenye benchi.
Kaseja alipata lawama nyingi baada ya kufungwa bao la kizembe kwenye mchezo wa Nani Mtani Jembe dhidi ya Simba ambao timu hiyo ya Jangwani ililala kwa mabao 3-1.
Kwenye mchezo wa juzi ambao Yanga ilishinda 2-1, Kaseja alikuwa jukwaani huku langoni akikaa  Deogratius Munishi na kipa namba mbili akawa Ally Mustapha ‘Barthez’. “Mimi ni mzima wa afya, siumwi na wala sina tatizo lolote, sioni kama ni ishu kubwa sana mimi kukosekana kwenye mechi ile.
“Nilikuwepo uwanjani lakini sikuwepo kwenye benchi, achana na hizo ishu bwana, mimi nipo na nipo poa kabisa.
“Kwani ni mimi tu sikuwepo? Hao wengine umewauliza kwa nini hawakuwepo? Labda uwaulize viongozi, mimi siwezi kuzungumza kitu chochote,” alisema Kaseja kwa kusitasita.
Kocha wa Yanga, Mholanzi, Hans van Der Pluijm alipoulizwa kuhusiana na kutomtumia Kaseja alisema: “Mimi niliangalia suala la kiwango, hasa walichokionyesha wachezaji tukiwa kambini Uturuki, kwa hiyo waliocheza ndiyo walionivutia zaidi.”


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...