Nyota Simba waomba usajili Yanga

Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji akihojiwa na wanahabari.
Na Wilbert Molandi
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, baadhi ya wachezaji wa Simba wamepiga hodi kwenye Klabu ya Yanga na kuomba kusajiliwa na timu hiyo.
Usajili wa ligi kuu unatarajiwa kufunguliwa Juni 16 na kumalizika mapema Agosti, mwaka huu.
Kwa mujibu wa chanzo cha habari kutoka ndani ya uongozi wa Yanga, wengi wa wachezaji ni wale ambao mikataba yao imemalizika na hawana uhakika wa kubaki kuendelea kuichezea Simba.
Chanzo hicho kimesema kuwa wachezaji hao mara kwa mara wanawapigia simu viongozi wa Yanga wakiomba kusajiliwa na timu hiyo.
“Kiukweli tunapokea simu nyingi kutoka kwa baadhi ya wachezaji wa Simba ambao sitaweza kuwataja, wakiomba kusajiliwa na Yanga.
“Kati ya wachezaji hao, wengi wao ni wachezaji huru ambao mikataba yao imemalizika mwishoni mwa msimu huu ambao wana hofu ya kutoongezewa mikataba mipya.
“Kama viongozi tunazungumza na kuwasikiliza tu wachezaji hao kwa sababu kila kitu kina mipango yake, kikosi chetu hakihitaji kuboreshwa kwa kuongeza wachezaji kwa sababu timu yetu bado ni bora.
“Katika kikosi chetu sehemu zinazohitaji kufanyiwa maboresho ni safu ya ulinzi, beki namba tatu, kiungo na washambuliaji wenye uwezo mkubwa wa kufunga mabao,” kilisema chanzo hicho.
Katika siku za hivi karibuni, Championi lilifanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Yanga, Beno Njovu, kuhusiana na usajili na kutamka kuwa hivi sasa wapo kwenye mazungumzo na baadhi ya wachezaji kwa ajili ya kuwasajili.
Naye Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji, alisema katika usajili wa msimu ujao, wamepanga kusajili wachezaji watano pekee, kati ya hao wawili kutoka nje ya nchi na watatu wazawa.
Wachezaji waliomaliza mikataba ya kuichezea Simba ni kiungo mshambuliaji Uhuru Selemani, Ramadhani Chombo ‘Redondo’, Yaw Berko na Haruna Shamte


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...