SHULE YA SEKONDARI YA WAMA-NAKAYAMA WAPEWA MSAADA WA BASI

IMG_3946Anna Nkinda – Maelezo

Shule ya Sekondari ya WAMA-Nakayama inayomilikiwa  na Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) imepatiwa msaada wa basi na kampuni ya Ashok Leyland ya jijini Dar es Salaam.Makabidhiano ya basi hilo yamefanyika leo katika viwanja vya Taasisi hiyo iliyopo wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam.Akiongea mara baada ya makabidhiano hayo   Mwenyekiti wa WAMA Mama Salma Kikwete aliwashukuru viongozi wa kampuni hiyo kwa msaada walioutoa na kusema anaamini msaada huo wameutoa baada ya kuangalia vigezo maalum na kuwaomba kuzidi kuwa na  moyo wa upendo kwao na kwa  wadau wengine.Mama Kikwete ambaye pia ni Mke wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete alisema Taasisi ya WAMA inafanya kazi mbalimbali zinazoonekana na jamii moja wapo ikiwa ni elimu na katika hilo wanashule ya Sekondari ya WAMA-Nakayama ambayo ni ya watoto yatima na wanaoishi katika mazingira hatarishi iliyoko wilaya ya Rufiji mkoani Pwani ambayo inawanafunzi 335 wa kidato cha kwanza hadi cha nne.

“Wenzetu hawa wametoa basi ambalo litasaidia kutatua changamoto ya usafiri shuleni  kwani wanafunzi kama wanafunzi wanashughuli zao za ndani na nje ya Shule. Kwa ukubwa wa basi hili tatizo la usafiri litakuwa limepungua kwa kiasi kikubwa kwakuwa  kabla ya kupata basi hili kulikuwa na lingine dogo”, alisema Mama Kikwete.
Kwa upande wake Bhimasena Rau ambaye ni Mkurugenzi Mwendeshaji Kimataifa kutoka kampuni ya Ashok Leyland alimpongeza Mama Kikwete kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuisaidia jamii wakiwemo wanawake na watoto hapa nchini na kusema kuwa wametoa basi hilo ambalo litasaidia katika kazi za kijamii.
Taasisi ya WAMA ilianzishwa mwaka 2006 inafanya  kazi katika eneo la elimu ya mtoto wa kike, afya, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuangalia watoto yatima na wanaoishi katika mazingira hatarishi


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...