RAY C AJIPONGEZA KUIPA KISOGO MIHADARATI

MSANII wa muziki wa kizazi kipya, Rehema Chalamila ‘Ray C’ mwishoni mwa wiki aliandaa sherehe kujipongeza kutimiza mwaka mmoja tangu aanze kutumia dawa za ‘methadone’ ambazo zimemsaidia kupona uraibu uliotokana na matumizi ya mihadarati.
Ray C, aliyabainisha hayo Dar es Salaam juzi, alipokuwa akizungumza na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Jumanne Sigini, alipotembelea Kituo cha Tiba cha Dawa za Kulevya (Methadone Wing), kilichopo katika hospitali ya Mwananyamala, Kinondoni.
Alisema ameamua kufanya hivyo kama shukrani zake baada ya kupona ugonjwa huo, ambao hapo awali ulimfanya apoteze mali nyingi na mwelekeo wa maisha yake.
“Leo tarehe nane natimiza mwaka tangu nianze kutumia methadone, hivyo nimeamua kufanya sherehe ndogo na wenzangu ‘rafiki’ katika kituo hiki, nimenunua vinywaji baridi na vitafunwa kidogo kwa ajili ya kufurahi pamoja, karibuni sana,” alisema Ray C na kuongeza.
“Sasa najisikia vizuri na namshukuru baba (Rais Kikwete), kwa kunishauri pamoja na jitihada zake za kuwaleta Wamarekani katika kutupatia tiba hii ambayo imenirudisha katika hali yangu ya kawaida, hadi nikaweza kuingia tena studio kurekodi nyimbo tena, ni jambo kubwa sana na la kujivunia,” alisema Ray C.
Aidha, Ray C aliitaka serikali kuongeza jitihada za mapambano yake, kwani janga hilo ni kubwa nchini kutokana na ukweli kwamba, wapo hata baadhi ya vigogo wanaotumia uraibu huo.
Alitoa rai kwa wasanii wenzake, wakiwemo wa filamu na baadhi ya watu maarufu ambao wamekwishaathirika na wanataabika na maumivu, wasione haya wajitokeze katika kituo hicho, kwani dawa ya methadone inaponesha.
Aidha, aliwaasa viongozi mbalimbali nchini kuunga mkono juhudi za Rais Jakaya Kikwete za kupambana na kutokomeza janga la uingizaji na utumiaji wa mihadarati kwa vijana.
Naye Katibu Mkuu wa Tamisemi, Sagini, aliiagiza Manispaa ya Kinondoni kuangalia uwezekano wa kuwapatia ajira baadhi ya vijana hao waliopona kutokana na elimu waliyonayo, kwani katika kundi hilo walikuwepo hata wasomi wa elimu ya ngazi ya chuo.
Naye mtaalamu katika kitengo hicho, Dk. Elias Mrita, alisema hadi sasa kuna wagonjwa 375 ambao hupatiwa matibabu na wapo ambao tayari wamekwishapona, na kwamba kituo hicho kinaendeshwa kwa msaada wa Serikali ya Marekani.


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...