KASHFA YA UZINZI:. LISSU AMSAFISHA MBOWE

Ojuku Abraham na Jelard Lucas
KATIKA kile kinachoonekana kama kumsafisha Mwenyekiti wa Taifa wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Freeman Mbowe dhidi ya kashfa ya uzinzi inayomuandama, Mwanasheria Mkuu wa chama hicho, Tindu Lissu amesema suala hilo ni maisha binafsi ya mtu, ambayo hayawezi kuhusishwa na wadhifa wake kwa namna yoyote.
Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tindu Lissu.
Akizungumza katika mahojiano maalum ndani ya chumba cha habari cha Global Publishers Ltd, Bamaga, Mwenge jijini Dar es Salaam juzi, Lissu alisema kwa kadiri anavyofahamu, suala hilo ni binafsi linalopaswa kuachwa chumbani, kwa sababu kama litahusishwa na nafasi yake, ni sawa na kukubali kuwa mzee Nelson Mandela wa Afrika Kusini si lolote wala chochote.
“Maisha ya kimapenzi ya mzee Mandela yalikuwa ya ukakasi, kwa maana hiyo unataka tuseme kuwa kwa sababu hiyo, mzee huyu hakuwa kiongozi bora, unataka tuseme Bill Clinton wa Marekani hakuwa kiongozi bora kwa sababu tu alipata kashfa katika moja ya makorido ya Ikulu ya White House? Mimi nadhani haya mambo kama yapo au hayapo, hayahusiani na uwezo wa mtu kiuongozi, ni mambo ya chumbani yanayopaswa kuachwa huko,” alisema Lissu.
Mwenyekiti wa Taifa wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Freeman Mbowe.
Lissu alikuwa akirejea baadhi ya sababu zilizosababisha  mgogoro kati ya chama chake na Naibu Katibu Mkuu wao aliyetimuliwa, Zitto Kabwe, anayedaiwa kushiriki kuandaa waraka wenye nia ovu, ambao pamoja na mambo mengine, ulitaka kufanyika kwa mabadiliko ya viongozi wa juu, akiwemo Mwenyekiti wa Taifa, kwa kudaiwa kuwa na elimu ndogo pamoja na kukosa uaminifu katika ndoa yake.
Aidha, hivi karibuni wakati wa kikao kilichomalizika cha Bunge mjini Dodoma, Freeman Mbowe alidaiwa kuvuruga ziara ya mbunge mmoja mwanamke (wa viti maalum) wa chama chake aliyekuwa katika ziara ya kibunge nje ya nchi, na badala yake kumtaka kuungana sehemu alipokuwepo.
Mbunge huyo wa Singida Mashariki, licha ya kukiri kuwepo kwa mgogoro unaokitikisa chama chao, lakini alisema hatimaye Chadema itashinda na kubakia imara na akasisitiza kuwa mwavuli wa mahakama alionao Zito ukiondoka, watamtimua.


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...